HUKU mataifa duniani yakiendelea na
siku 16 za kupinga udhalilishaji wa kijinsia, mambo yamegeuka Zanzibar ambapo wanawake wanadaiwa
kuwanyanyasa wanaume.
Kwa ilivyozoeleka wanawake ndio
waathirika wakubwa wanaokabiliwa na vitendo vya udhalilishaji, lakini hapa Zanzibar kibao
kimewageukia wanaume ambao kwa mujibu wa jeshi la Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi
zipo kesi kadhaa zilizoripotiwa.
Akizungumza Ofisini kwake Muembemadema, Mkuu wa Dawati hilo Staff Sagenti Zahor Faki, alisema
kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wanawake wenye tabia ya kuwanyanyasa
waume zao ikiwemo kuwapa vipigo.
Alisema dawati lake limepokea
kesi tisa za wanawake kuwadhalilisha wanaume na kwamba kesi hizo zimeripotiwa
kuanzia mwezi Januari mwaka huu hadi Oktoba.
Alisema wanawake wengi wenye kufanya
vitendo vya udhalilishaji hasa vya kuwapiga waume zao, hufanya kwa kuvizia hasa
wakiwa wanaume hao wamelala.
Mkuu huyo alisema sababu kubwa
zinazopelekea waume hao kupigwa na wake zao zinatokana na wanawake wengi kuwa
na wivu wa kupindukia katika ndoa zao pamoja na migogoro ya kugombani mali.
Aidha akizitaja sababu nyengine alisema
zinatokana na watoto wakati wazazi wao wanapoachana huku mwanamke akizuia hati
ya nyumba ambayo si haki yake bila kukaa kulitatua tatizo hilo.
"Sababu hii inatokana na mume
alieachana na mke wakati wakiwa wameshazaa mwanamke huanza vurugu na kuzuia
hati ya nyumba wakati si haki yake na husema hatoi mpaka apewe kitu fulani bila
ya kukaa pamoja na kulitatua tatizo hilo",
alifafanua Mkuu huyo.
Alifahamisha kuwa wanawake wengi
wamekuwa wakiwavizia waume zao wakati wakiwa usingizini na kuwajeruhi sehemu
mbalimbali za miili ikiwemo sehemu ya siri huku wakiwapa maneno makali.
0 comments:
Post a Comment