Nov 25, 2013

Elimu Ya NGONO Mashuleni Ina Hamsha Hisia Za Ngono.

SHIRIKA la Kimataifa la Kutetea Uhai wa Binadamu, tawi la Tanzania (Prolife Tanzania), limesema elimu ya ngono inayofundishwa shuleni, inapandikiza mbegu za uasi dhidi ya uzazi na uzao.

Mkurugenzi wa shirika hilo Tanzania na Nchi za Afrika zinazungungumza lugha ya Kingereza, Emil Hagamu alisema elimu hiyo, inahimiza mauaji ya watoto wachanga kabla ya hawajazaliwa.

Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki na kuhimiza kuwa, malezi bora kwa watoto kulingana na mafundisho ya dini ni njia ya kuwaepusha na vitendo vinavyochochea ngono na wala si vinginevyo.

“Katika elimu ya ngono watoto wanafundishwa viungo vya uzazi na jinsi vinavyofanya kazi. Wanafundishwa ‘vitendo vya wakubwa’ na jinsi mimba inavyotungwa,” alisema.

“Masomo hayo yanaamsha hisia za kingono miongoni mwa wanafunzi na kuwajengea udadisi wa kutaka kujaribu,” alisema Hagamu.

Alisema baada ya kuamsha hisia na vionjo vyao vya ngono, walimu wa somo la ngono wanawapatia wanafunzi zana za kufanyia ngono bila hofu.

“Wanawaeleza wanafunzi hao kuwa, wapo maadui wawili katika elimu yao ambao ni mimba na magonjwa ya zinaa.
“Ili kuepuka mimba na magonjwa ya zinaa, lazima watumie vidhibiti mimba. Kwa hiyo tangu utotoni wanafundishwa kuwa,  mimba ni kitu cha hatari kinachotakiwa kuepukwa kwa gharama zozote.

“Kwa vile vidhibiti mimba vina viwango vya kushindwa, basi msichana anapopata mimba anashauriwa kwenda kutoa ili aendelee na masomo,” alisema.

Alitolea mfano mhudumu mmoja aliwarubuni wanafunzi wa sekondari fulani jijini Dar es Salaam kwa swali hili, “nani kati yenu yuko tayari kuwaaibisha wazazi wake kwa kukosa masomo kutokana na mimba?”

Alisema kuwa, kila msichana alijibu kwa sauti kubwa, “hakuna” basi yule mhudumu aliyetoka shirika fulani la nje lisilo la kiserikali akawaambia chagueni moja ya njia zilizopo, vidonge vya majira, sindano za depo provera, vipandikizi, vitanzi au kondomu.
Alifafanua kuwa, wanafunzi hao walichagua walichokitaka na baada ya kutumia, licha ya kupata madhara, walifeli pia masomo, na wengine walikosa uwezo wa kuzaa hadi sasa.

“Mbaya zaidi mhujumu yule aliwatengenezea wasichana hawa mazingira mazuri ya kuwa waasherati na kuwaweka katika hatari ya kuambukizwa magonjwa ya zinaa, ukiwemo ukimwi,” alisema.

Alitanabiasha kuwa, kuhusu madhara ya elimu ya ngono shuleni,wataalamu mbalimbali waliwahi kusema, “vitendo vya ngono miongoni mwa watoto vinaongezeka kwa kadiri elimu hiyo inavyofundishwa, kwa kadiri elimu hiyo inavyotolewa katika umri mdogo ndivyo watoto wanavyojiingiza katika vitendo vya ngono katika umri mdogo”.

Alisema vitendo holela vya ngono husababisha mimba katika umri mdogo na kuongeza miongoni mwa watoto wa shule ndivyo, vitendo vya utoaji mimba au utupaji wa watoto vinavyoongezeka.

Prolife inaamini kuwa, utaoji mimba ni mauaji kama yalivyo mauaji mtu mzima.

0 comments:

Post a Comment