Sep 25, 2013

Mtambo Wa Usimamizi Wa Masafa Wazinduliwa ZANZIBAR


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kasi ya uwekezaji nchini inaweza kuongezeka mara dufu iwapo wananchi watazingatia zaidi uimarishaji wa mazingira hasa katika mtandao wa mawasiliano.

Alisema wawekezaji wengi huvutika na hali ya mazingira safi yanayowashawishi kupanua wigo wa mtandao huo ambao husaidia kupatikana kwa huduma zote za msingi za mawasiliano kwa upande wa simu, posta na utangazaji.
Balozi Seif alieleza hayo wakati akizindua mtambo maalum wa usimamizi wa masafa ya mawasiliano Zanzibar hafla iliyofanyika katika Ofisi ya Mamlaka ya mawasiliano Tanzania { TCRA } iliyopo Chukwani nje kidogo ya Maji wa Zanzibar.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanzisha mfuko wa mawasiliano kwa wote ili kuunga mkono juhudi za wawekezaji binafsi na washirika wa maendeleo katika ujenzi wa miundo mbinu ya mawasiliano kwenye maeneo ya vijijini ambayo kibiashara bado hayajavutia wawekezaji.

Alieleza kwamba Serikali imefanya hivyo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010 na Dira ya Taifa ya Tanzania ya mwaka 2015.

Balozi Seif alisema ujio wa wawekezaji hao umesaidia kwa kiasi kikubwa kupungua kwa gharama za mawasiliano ya simu na utangazaji ikiwa ni pamoja na kuongeza pato la Taifa.

“ Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imefarajika kwa kutimiza wajibu wenu na kuhakikisha kuwa Zanzibar pia inakuwa na uwezo wa kusimamia masafa muda wote bila ya kusubiri mtandao kama huo kutoka Tanzania Bara “. Alisisitiza Balozi Seif.
“ Nafurahi kuona Tanzania hivi sasa inajipanga kwenda kisasa zaidi “. Alifafanua Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

0 comments:

Post a Comment