Nov 18, 2013

WAFANYA BIASHARA WAGOMA DAR


BAADHI YA MADUKA MTAA WA SWAHILI YAKIWA YAMEFUNGWA.

Wafanya biashara wa maduka mbalimbali katikati ya jiji la Dar es salaam wamegoma.

Hayo yamebainika Asubuhi wakati munira blog ilipotembelea mitaa kadhaa na kukuta maduka hayo yakiwa yamefungwa.

Wakiongea na munira blog baadhi ya wafanya biashara hao wamedai kwamba wamechoshwa na unyanyasaji unaofanywa na Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA kwa kuwalazimisha watumie risiti za mashine ya TRA.
Wakiongea kwa sharti la kutotaja majina wala kupigwa picha,wafanya biashara hao wa Maeneo ya Kariakoo mtaa wa Nyamwezi walisema,wao wananua nguo shilingi elfu kumi na wanaiuza kati ya shilingi elfu kumi na moja hadi kumi na mbili,papo hapo wanakatwa kodi ya asilimia kumi nane kitu ambacho ni hasara kwao.

Wakiongea kwa hasira walisema "huu ni uonevu tunalazimishwa tuzinunue mashine hizo kwa shilingi laki nane wakati china zinauzwa kwa dola hamsini".

Waliongeza kwa kusema "msimamo wetu ni kwamba hatuzitaki mashine hizi hata tukipewa bure",mwisho wa kuwanukuu.

Kwa upande wake Bwana Abdul Aziz Ramadhan Tosira mfanya biashara wa nguo amesema mashine za TRA haziendani na mazingira halisi ya wafanya biashara wadogo zaidi ya kuuwa biashara zao.

Alitolea mfano kwa nchi ya china na india kwamba mashine hizo hazitumiki kwa wafanya biashara wadogo.

"Bora warudishe utaratibu wa zamani wa kila mfanya biashara kulipa shilingi laki mbili na elfu sabini na nne kwa mwaka mzima,bila ya hivyo mgomo huu utakuwa mkubwa zaidi"Mwisho wa kumnukuu.

Munira blog imedokezwa kwamba mgomo huu utadumu kwa siku tatu kwa lengo la kuishinikiza Serikali kufuta utaratibu wa matumizi ya risiti za mashine kwa wafanya biashara wadogo.

Tayari taharuki imezuka katikati ya jiji kutokana na baadhi ya wafanya biashara waliokuwa tayari kufungua maduka kulazimishwa kufunga maduka yao na kundi la watu kama alivyo shuhudia mwandishi wa habari hizi katika mitaa ya Swahili Kariakoo Dar es salaam.

Viongozi wa wafanya biashara hao wala kamishna wa mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) hawakuweza kupatikana kuzungumzia mgomo huo ambao tayari umeshaanza kuwaathiri walaji.

 MFANYA BIASHARA ABDUL AZIZ RAMADHAN TOSIRE AKIHOJIANA NA MUNIRA BLOG.
  MADUKA MTAA WA AGGREY YAKIWA YAMEFUNGWA.

MADUKA YA MTAA WA NYAMWEZI YAKIWA YAMEFUNGWA.

0 comments:

Post a Comment