Sep 25, 2013

MISRI kuwekeza Zanzibar


Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesifu hatua ya Misri kutaka kuleta miradi ya uwekezaji katika sekta ya uvuvi wa bahari kuu visiwani Zanzibar, kwa vile sekta hiyo itatoa fursa nyingi za ajira na kuinua uchumi wa serikali na wananchi.

Maalim Seif ameyasema hayo jana ofisini kwake Migombani mjini Zanzibar, alipofanya mazungumzo na Balozi mdogo wa Misri Zanzibar, Walid Mohammed Ismail.

Alisema Zanzibar ina utajiri mkubwa wa maliasili za baharini ambazo hazijatumika ipasavyo kuinua uchumi na maisha ya Wazanzibari, hivyo hatua ya kukaribisha uwekezaji katika sekta ya uvuvi wa bahari kuu ni muhimu kwa wakati huu.

Alisema iwapo miradi ya uvuvi inayokusudiwa kuanzishwa na kampuni za Misri italeta mafanikio, wananchi wengi hasa vijana watanufaika na ajira na hivyo kuondokana na ugumu wa maisha unaojitokeza.

Mapema, balozi huyo mdogo, alimueleza Makamu wa Kwanza wa Rais kuwa mipango ya kuwawezesha wawekezaji katika uvuvi wa bahari kuu kuja Zanzibar inaendelea na kwamba ujumbe kutoka Misri unatarajiwa kuwasili mwezi ujao.

Balozi huyo alisema atawashawishi wawekezaji watakaofika Zanzibar kuweka umuhimu mkubwa katika kufungua viwanda vya kusindika samaki na mazao mengine ya baharini, ili kutoa fursa kubwa zaidi ya ajira kwa wananchi.



0 comments:

Post a Comment