HAPA RAIS UHURU KENYATA AKILIHUTUBIA TAIFA NA KUTANGAZA KUMALIZIKA KWA MAPAMBANO KATI YA SERIKALI NA KUNDI LA AL SHABBAAB
Kundi la Al-Shabaab limedai siku ya Jumatano kuwa mateka 137
waliowachukua wamekufa katika uvamizi wa kituo cha biashara, idadi
ambayo ni vigumu kuithibitisha na kubwa kuliko idadi iliyotangazwa kuwa
hawajulikani walipo.
Wapiganaji hao walio na mafungamano na mtandao wa Al-Qaeda, katika
ujumbe waliouweka katika mtandao wa kijamii wa twitter, walisema mateka
137 waliokuwa wanashikiliwa na mujahedeen walikufa.
Waliwashtumu pia
wanajeshi wa Kenya kwa kutumia vifaa vya kemikali kukomesha mkwamo huo
uliodumu kwa siku nne. "Katika hatua ya uoga wa dhahiri, vikosi vya
Kenya kwa maksudi vilitumia vilipuzi vilivyokuwa na kemikali," ulisema
ujumbe mmoja na kuongeza kuwa, "ili kufunika uhalifu wao, serikali ya
Kenya iliendesha zoezi la kuliporomosha jengo, na kuuzika ushahidi na
mateka wote chini ya vifusi."
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, alitangaza kumalizika kwa umwagaji huo wa
damu uliodumu kwa saa 80 jioni ya Jumanne, ambao ulisababisha vifo vya
raia 61 na maafisa sita wa vikosi vya usalama.
Polisi ilisema idadi hiyo
ya vifo ingeweza kuongezeka, ambapo shirika la misaada la Msalaba
mwekundu liliorodhesha watu 63 ambao bado hawajulikani walipo.
Hakukuwa
na kauli kutoka serikali ya Kenya kuhusiana na madai hayo ya
Al-Shabaab waliyoyatoa kupitia kwenye mtandao wa twitter.
Wanajeshi wa ulinzi wa Kenya wakijiandaa kuingia jengo la Westgate kupambana na wavamizi.
Kundi hilo lilisema lilifanya shambulizi hilo katika kulipiza kisasi
dhidi ya Kenya kutokana na kujiingiza nchini Somalia kupambana na
wanamgambo hao.
Katika moja ya mashambulizi mabaya zaidi katika historia
ya Kenya, wapiganaji hao waliingia katika jengo la maduka la Westagate
lenye ghorofa nne, ambalo linamilikiwa kwa sehemu na raia wa Israel,
mchana wa Jumamosi, na kuanza kuwashambulia wanunuzi kwa risasi na
kuripua maguruneti.
Kenya ilianza siku tatu za maombolezi rasmi Jumatano, ambapo bendera za
taifa zinapepea nusu mlingoti, huku wafanyakazi wa uokozi wakisafisha
mabaki ya jengo la Westgate kutafuta miili ya wahanga wa tukio hilo.
Karibu watu 200 walijeruhiwa katika uvamizi huo wa siku nne, ambao
ulishuhudia mapambano makali kati ya wapiganaji na vikosi vya usalama
vya Kenya katika jengo hilo, ambalo ndicho kituo kikubwa zaidi cha
biashara na maarufu kwa watu wenye uwezo nchini Kenya, wanadiplomasia,
wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa na watalaamu wengine.
Picha kwa hisani kubwa ya Reuters.
0 comments:
Post a Comment