Oct 3, 2014

Shekau: Sijauawa na jeshi la Nigeria ningali hai

Kiongozi wa kundi la kitakfiri na kigaidi anayedaiwa kuitwa Abubakar Shekau, ametokeza hadharani na kukadhibisha habari zilizoenezwa na mitandao mbalimbali za kuuawa kwake na jeshi la Nigeria.
Akizungumza kupitia njia ya video yenye dakika 36 Shekau amesema kuwa, yeye angali hai na kwamba wapiganaji wake wanaendelea kuikalia miji waliyoidhibiti kutoka kwa jeshi la serikali ya Nigeria. 

Tarehe 24 mwezi uliopita, jeshi la Nigeria lilitangaza habari ya kuuawa kiongozi huyo wa kundi la kitakfiri la Boko Haram. Itakumbukwa kuwa, mwaka 2009 duru za kiusalama nchini humo zilitangaza pia kuuawa kiongozi huyo anayeitwa Abubakr Shekau, bila kutangazwa rasmi habari hiyo na jeshi la nchi hiyo. 

Boko Haram ambalo ni kundi lenye misimamo ya kufurutu mipaka ya mafundisho sahihi ya Uislamu, limeitumbukiza Nigeria kwenye dimbwi la machafuko na mauaji sambamba na kuzusha hitilafu za kidini na kikabila nchini humo. 

 Baadhi ya weledi wa mambo wanasema Boko Haram lina mahusiano ya moja kwa moja na viongozi wa juu wa serikali ya Nigeria wenye lengo la kutumia hujuma za kundi hilo kufikia malengo yao ya kuendelea kusalia zaidi madarakani.

0 comments:

Post a Comment