Suala la Mahakama
ya Kadhi limechafua hali ya hewa bungeni mjini Dodoma baada ya wajumbe
Waislamu kutishia kupiga kura ya hapana kama halitaingizwa katika Rasimu
inayopendekezwa.
Wakati Waislamu wakishikilia msimamo huo, wajumbe
ambao ni Wakristo nao wamejipanga kupiga kura ya hapana endapo Mahakama
ya Kadhi itaingizwa katika Katiba inayopendekezwa.
Dalili za mpasuko huo zilianza kujitokeza jana
asubuhi baada ya mjumbe mmoja, Jaku Ayub Hashim kuwasha kipaza sauti
akitaka kuzungumza akisema ana jambo muhimu.
“Mheshimiwa tangu jana (juzi) ulisema utanipa
nafasi ya mwanzo nizungumze,” alisema Jaku, lakini Makamu Mwenyekiti,
Samia Suluhu alimtaka aketi chini na suala lake limesikika.
Suluhu akaendelea kuwapa wajumbe wengine kuendelea
kuchangia na baadaye alimpa Jaku muda wa dakika saba ili kuwasilisha
kile alichotaka kukizungumza ndani ya Bunge hilo.
Jaku alisema walipendekeza kifungu kinachotaka
uamuzi unaohusu ndoa, talaka na mirathi iliyoamuliwa kwa misingi ya dini
ingizwe kwenye Katiba inayopendekeza lakini hakimo.
“Ni kitu kidogo kabisa tuliomba kiongezwe lakini
cha kusikitisha kikundi cha sanaa kimeingizwa. Mimi binafsi yangu
sitaunga mkono wala mguu wala sitaipigia kura hii,” alisema Jaku.
Suluhu akamweleza kuwa angalizo lake
limechukuliwa, na uongozi wa Bunge pamoja na kamati ya Uandishi
wanajitahidi kuingiza kila kitu kinachowezekana, lakini kwa misingi na
sheria za nchi.
Baadaye Sheikh Masoud Jongo alipopewa nafasi ya
kuchangia, naye alitahadharisha kuwa mambo yaliyopendekezwa na Waislamu
yasipoingizwa kama ilivyo kwa sasa, hawatakuwa tayari kwa lolote.
“Msimamo wetu sisi Waislamu kama mambo yetu
tuliyoleta katika mapendekezo hayataingizwa, basi yatabomokea hapa na
hatutakuwa tayari tena,” alisema Sheikh Jongo, kauli iliyowashtua
wajumbe.
Akihitimisha majadiliano hayo, Mwenyekiti wa
Kamati ya Uandishi, Andrew Chenge alisema kamati yake imefanya kazi kwa
uadilifu mkubwa na kwa masilahi ya Watanzania.
Akiahirisha Bunge, Suluhu alisema kesho Bunge litaanza kwa kupitia baadhi ya mambo yaliyoibuka katika uhakiki kisha kupitisha azimio la upigaji wa kura.
Kura zitapigwa kati ya kesho hadi Oktoba 2.
Akiahirisha Bunge, Suluhu alisema kesho Bunge litaanza kwa kupitia baadhi ya mambo yaliyoibuka katika uhakiki kisha kupitisha azimio la upigaji wa kura.
Kura zitapigwa kati ya kesho hadi Oktoba 2.
Baada ya kuahirishwa kwa Bunge, Sheikh mwingine,
Hamid Jongo alimwendea Askofu mstaafu Donald Mtetemela na kumkumbatia,
kisha kumvuta pembeni na kisha kuteta kwa dakika tano.
0 comments:
Post a Comment