KUMCHAPA mwanafunzi kunaweza kumsababishia usugu utakaomfanya asijali
jambo lolote baya analokatazwa kwa kuwa atakuwa amezoea kuchapwa. Watoto
wa siku hizi wamekuwa na uelewa mkubwa wa mambo ukilinganisha na wa
zamani. Unaweza kukuta watoto wakimaliza shule ya msingi wakiwa wadogo
hivyo huingia sekondari wakiwa bado hawajakomaa. Hivyo, ili kuepuka
matatizo ya hapa na pale, adhabu wanazopewa ni muhimu ziendane na umri
wao.
Mwalimu anao uwezo wa kumrekebisha mwanafunzi hata kwa maneno tu.
Adhabu ya viboko kwa namna moja au nyingine si nzuri kwa watoto kwa kuwa
inaweza kusababisha madhara makubwa. Kama mwanafunzi ni mkaidi kupita
kiasi ni vema akapewa adhabu ndogondogo kama kufanya usafi katika uwanja
wa shule, darasani bila msaada wa wenzie, kufyeka nyasi, kufagia na
nyingine nyingi za aina hiyo.
Adhabu ya viboko humfanya mtoto kutokuwa mdadisi wa mambo. Humfanya ashindwe kuwa karibu na mwalimu kwa kuhofia kuchapwa.
Hivi
majuzi, shule moja mkoani Iringa Wilaya ya Makambako, mtoto wa darasa
la tatu baada ya kukosea kuandika herufi, mwalimu wake aliamua kumpiga
katika tezi za shingo na mgongoni kwa kutumia rula ya kupigia mstari
ubaoni. Baada ya kumpiga mwanafunzi huyo alifariki. Alipopelekwa
hospitali ikabainika chanzo cha kifo chake ni kipigo kutoka kwa mwalimu.
Alibainika akiwa na usaha na damu ilivilia katika ubongo wake.
Jambo kama hili linapotokea, mzazi huwa katika wakati mgumu.
Sasa
basi, kwa kuwa Serikali imeruhusu viboko kwa wanafunzi na ukizingatia
kuwa kila binadamu ana kiwango chake cha hasira, suala hili linaweza
kuleta hasara kubwa kwa wazazi kupoteza watoto wao hasa ukizingatia siku
hizi maradhi ni mengi.
Katika hali ya kawaida, ni rahisi mno kwa wazazi kujenga uhasama na walimu kutokana na vipigo wanavyopata watoto wao.
Baadhi
ya waalimu wamekua wakichapa watoto bila hata kuangalia ni eneo gani
analomchapa mwanafunzi.
Tumeshashuhudia wanafunzi wakitokwa na damu
puani kutokana na kipigo wanachopata kutoka kwa walimu. Suala kama hili
ni hatari kwa wanafunzi kwani athari zake ni kubwa kuliko kumfundisha
mwanafunzi kuwa na maadili mema shuleni na hata nyumbani.
Ikiwezekana
Serikali iangalie upya suala hili maana kuna watoto wanapata ulemavu
kutokana na viboko shuleni. Mkoani Iringa kuna mwanafunzi hadi leo hii
hawezi kutembea wala kujisogeza kutoka sehemu moja kwenda nyingine
kutokana na kuchapwa viboko visivyo na idadi tena bila utaratibu na
mwalimu wake.
Mtoto si nyoka hadi apigwe kichwani, haijalishi
ametenda kosa gani. Hivyo walimu wasijisahau pindi wanapowachapa watoto
wa wenzao kwa kuwa nao pia ni wazazi.
Tunafahamu kuwa viboko
shuleni vinasaidia kurekebisha wanafunzi hasa wale watukutu. Lakini
jambo la msingi walimu wanapaswa kuwachapa kwa utaratibu na wawe na
kiwango maalumu cha fimbo anachostahili kuchapwa mtoto kulingana na kosa
alilofanya, pia kuangalia umri wake kwani wengine huanza masomo wakiwa
na umri mdogo mno.
Walimu wanapaswa kuwa makini katika hili ili kuepuka lawama, vifo shuleni na uhasama baina yao na wazazi
Sep 20, 2013
Walimu Punguzeni Bakora
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment