Nov 2, 2013

Mwanafunzi wa Kiislamu Afanyiwa Unyama



MWANAFUNZI wa Chuo cha Slafia Bunju A, Dar es Salaam, Nasibu Chipoto (23), ameumia vibaya baada ya kudai kufanyiwa unyama na jirani ambaye ni raia wa Kongo.

Makamu Mkuu wa chuo hicho cha Kiislam, Abdallah Yusuf, alisema tukio hilo lilitokea Oktoba 28 mwaka huu, saa 3: usiku.

Yusuf alisema wanafunzi wa chuo hicho wana kawaida ya kuchota maji katika nyumba hiyo, hivyo siku ya tukio Chipoto alikwenda kuchota maji ndipo alipovamiwa na mmiliki wa nyumba hiyo na kumfunga kamba mikono na miguu na kuanza kumpa mateso.

Alidai mmiliki huyo kwa kushirikiana na mkewe na wafanyakazi wake watatu walimpiga kijana huyo huku wakimchoma na pasi ya umeme mwilini na kumsababishia maumivu makali.

Makamu huyo alidai baada ya kusikia kelele walikwenda eneo hilo, ili kumuokoa kijana huyo lakini mmiliki huyo alitoa bastola na kuwatishia ndipo wakaamua kukimbilia kituo cha polisi kutoa  taarifa.

“Kijana wetu alipata mateso makali; wale watu walimfunga mikono wakampiga huku yule mmiliki akimchoma na pasi mwili mzima. Mbaya zaidi akatutishia kwa kutufyatulia risasi tulipotaka kumuokoa,” alieleza.

Alidai wakiwa kituo kidogo cha polisi cha Wazo kabla hawajaondoka, mmiliki huyo alifika akiwa amembeba kijana huyo huku akidai kuwa ni mwizi.

Yusuf alidai kuwa kutokana na hali ya kijana huyo kuwa mbaya polisi walimweka chini ya ulinzi mmiliki huyo na kijana huyo kupewa PF3 na kwenda kutibiwa hospitali ya Mwananyamala.

“Tunamshukuru Mungu sasa Chipoto anaendelea vizuri na yuko kwa ndugu zake Mbagala ila huyu mtuhumiwa tunasikia ameachiwa kwa dhamana,” alidai.

Alipoulizwa Kamanda Wambura alisema hana taarifa juu ya tukio hilo na kuahidi kulifuatilia na kutoa taarifa.

0 comments:

Post a Comment