Feb 22, 2015

Wamarekani milioni 50 katika lindi la umaskini

Ikulu ya Marekani (White House) imesema katika ripoti iliyotumwa katika Kongresi ya nchi hiyo kwamba Wamarekani milioni 50 ambao ni sawa na asilimia 15 ya jamii ya watu karibu milioni 300 wa nchi hiyo, wanaishi katika umaskini.
Ripoti hiyo ya White House pia imesema kuwa tabaka la kati la raia wa nchi hiyo linasumbuliwa na mbinyo na mashinikizo kutokana na kutoongezeka mishahara licha ya kuboreka hali ya uchumi wa Marekani katika miaka ya baada ya mdororo mkubwa wa kiuchumi.

Wakati huo huo taasisi moja ya utafiti ya Ufaransa ilitangaza hivi karibuni kuwa, Marekani inashika nafasi ya kwanza kati ya nchi zilizoendelea kwa kuwa na idadi kubwa na watu maskini.

Mstari wa umaskini nchini Marekani ni pato la dola elfu 23 na 850 kwa mwaka kwa familia yenye watu wanne na inasemekana kuwa, aghlabu ya Wamarekani wenye umri wa kati ya miaka 25 hadi 75 huonja shubiri ya umaskini kwa miaka kadhaa. 

Kiwango cha umaskini huo huwa shadidi zaidi kwa Wamarekani weusi wenye asili ya Afrika na familia zenye mzazi mmoja.

Takwimu mpya na rasmi za serikali ya Marekani zinaonesha kuwa, asilimia 16 ya watoto wa Kimarekani wanaishi chini ya mstari wa umaskini. 

Katika ripoti yake ya hivi karibuni, Kituo cha Takwimu cha Marekani kilitangaza kuwa, idadi ya watoto wa Marekani ambao familia zao zinatumia vibali maalimu vya msaada wa chakula kutokana na umaskini wa kupindukia, imeongezeka maradufu katika kipindi cha miaka saba iliyopita.
 
Wakati huo huo Shirika la Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF) limetangaza kuwa Marekani inashikilia nafasi ya pili kati ya nchi zinazoongoza kwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya watoto maskini kati ya nchi zilizoendelea. 

Vilevile ripoti mpya ya jumuiya isiyo ya kibiashara ya "Elimu na Malezi Kusini" ya huko huko Marekani inasema zaidi ya nusu ya wanafunzi wanaosoma katika shule za serikali wanastahiki kupewa msada wa chakula na mahitaji mengine ya kimaisha au kwa bei ya ruzuku. 

Ripoti ya jumuiya hiyo inasema thuluthi mbili ya majimbo ya kusini mwa Marekani inakabiliwa na umaskini mkubwa ulioenea kati ya wanafunzi.

Licha ya ripoti hizo zote zinazoonesha kiwango kikubwa cha umaskini nchini Marekani lakini serikali ya nchi hiyo imezidisha mazingatio yake kwenye miradi yenye gharama kubwa ya kijeshi na kijasusi ndani na nje ya nchi hiyo.

 Gazeti la Financial Times la Marekani limeandika kuwa nchi hiyo ilitumia zaidi ya dola trilioni mbili na bilioni 700 katika vita vya Afghanistan na Iraq. 

Hii ni katika hali ambayo bajeti ya mwaka 2014 ya Marekani ilikuwa dola trilioni 3 na bilioni 77. 

Bajeti ya masuala ya kijeshi ya Marekani katika mwaka huu wa 2015 ni dola bilioni 585.

Wataalamu wanasema kuwa iwapo nusu tu ya kiwango hicho cha bajeti ya masuala ya kijeshi ya Marekani itatumiwa kama misaada ya kifedha au kwa ajili ya kutayarisha nafasi mpya za ajira basi mamia ya maelfu ya raia wa Marekani wataondoka chini ya umaskini wa kutupa.

0 comments:

Post a Comment