Feb 21, 2015

Kiongozi wa vijana JKT atekwa, aokotwa


Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Ernest Mangu 

Utata umezingira suala la kijana George Mgoba, ambaye amekuwa akijitambulisha kuwa kiongozi wa wahitimu wa mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) baada ya habari kuwa alitekwa na baadaye kutupwa kwenye Msitu wa Pugu, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.


Si Jeshi la Polisi mkoani Pwani wala Dar es Salaam lililokuwa tayari kuzungumzia tukio la kijana huyo kutekwa, kupigwa na kutekelezwa kwenye msitu huo, lakini msemaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MHN) alithibitisha kuwapo kwa kijana huyo hospitalini hapo kuanzia jana saa 10:30 jioni, ingawa hakutaka kutoa maelezo mengi.

Mgoba amekuwa akihamasisha vijana wenzake waliohitimu ya JKT kukusanyika jijini Dar es Salaam na kuandamana hadi kwa Rais ili kumweleza masikitiko yao ya kutopatiwa ajira baada ya kumaliza mafunzo kama walivyoahidiwa wakati wakienda kwenye kambi za jeshi hilo.

“Ndio aliletwa hapa majira ya saa 10:30 akitokea Hospitali ya Amana,” alisema ofisa uhusiano wa MHN, Aminiel Aligaeshi.

“Lakini waganga walipotaka kumtibu alikataa kwa sharti kwamba atibiwe wakati ndugu zake wakiwapo. 

Ndugu zake walipofuatwa nje, hawakuonekana. Anaonekana ana maumivu sehemu ya mgongoni na anapumua kwa shida.”

Habari zinasema kuwa kuanzia saa 1:00 jioni madaktari walikuwa wakijaribu kumshauri akubali kutibiwa, lakini akakataa na hivyo kuwalazimu madaktari kumtaka asaini fomu ya kukataa matibabu.

 Hata hivyo hadi saa 2:00 usiku hakuwa amesaini.

Kijana huyo anasemekana kutekwa juzi jioni na watu ambao hawajajulikana na aliokotwa na msamaria mwema ambaye baadaye aliungana na watu wengine kumpeleka Hospitali ya Tumbi.

Hata hivyo, aligoma kutibiwa kwenye hospitali hiyo akitaka ndugu zake wawepo.

Habari zinasema baadaye alisafirishwa kuhamishiwa Hospitali ya Amana kabla ya kuhamishwa tena na kwenda Muhimbili jana saa 9:00 alasiri.

Mfanyakazi mmoja wa Hospitali ya Amana aliiambia gazeti hili kuwa kabla ya askari wa Jeshi la Polisi kumfuata na gari mbili aina ya Land Rover, kundi la vijana wanaosadikiwa kuwa ni wahitimu wa mafunzo ya JKT, liliwasili Amana na kutaka kushinikiza kumchukua Mgoba, lakini uongozi uliwakatalia kwa maelezo kuwa wangetoa ruhusa hiyo kama wangekuwapo ndugu zake.

Alivyotekwa

Mwandishi wetu kutoka Kibaha anaripoti kuwa kijana huyo, anayejielezea kuwa ni mtetezi wa vijana waliohitimu JKT, aliokotwa kwenye kichaka kilichopo Picha ya Ndege mjini humo akiwa amejeruhiwa maeneo mbalimbali ya mwilini.

0 comments:

Post a Comment