Apr 17, 2014

UNICEF imetoa wito kuachiliwa kwa watoto wa shule waliotekwa nyara Borno, Nigeria



Shirika la watoto duniani UNICEF limelaani ripoti za kutekwa nyara wasichana  mia moja wa shule walio kati ya umri wa miaka 12 hadi 17 kutoka shule ya Chibok jimboni Borno usiku wa Jumatatu na kutaka waachiliwe mara moja.

UNICEF imesema inasikitishwa na visa vya mashambulizi shuleni nchini Nigeria.

Hivi majuzi watu wasiojulikana waliokuwa wamejihami waliwauwa watoto 53 walio kati ya umri wa miaka 13 hadi 17 katika chuo cha elimu cha serikali, Buni Yadi katika jimbo la Yobe mwezi Februari

Halikadhalika UNICEF imesema kwamba vitendo vya ukatili kama hivyo havikubaliki huku ikisema kwamba vinawanyima watoto fursa ya kusoma katika mazingira salama na hivyo kuhatarisha mustakbali wa maisha yao.

Utekaji nyara wa watoto umetajwa kama kosa na ukiukwaji wa sheria za kimataifa.

 Shambulizi la Jumatatu shuleni Chibok lilifanyika saa chache baada ya shambulizi la bomu katika kituo cha basi karibu na mji mkuu,Abuja ambako takriban watu 70 walipoteza maisha.

UNICEF imeelezea mshikamano wake na jamii ya waathirika wa vitendo hivyo na familia za watoto waliotekwa nyara wakati huu mgumu na kutoa wito kuimarishwa kwa ulinzi wa watoto.

0 comments:

Post a Comment