Apr 2, 2014

UN yajiandaa kuwahamisha Waislamu 19,000 CAR

Umoja wa Mataifa umeeleza kuwa unajiandaa kuwahamisha Waislamu wapatao 19,000 ambao wanakabiliwa na hatari ya kushambuliwa na wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka huko Jamhuri ya Afrika ya Kati. 

Fatoumata Lejeune-Kaba Msemaji wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) amewaambia waandishi wa habari huko Geneva Uswisi kuwa, shirika hilo halitaki kuona  watu wakiuliwa.
Amesema kuwa wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka wanadhibiti njia kuu za kuingilia na kutoka katika mji mkuu Bangui na pia idadi kadhaa ya miji na vijiji huko kusini magharibi mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Msemaji wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa ameongeza kuwa wanamgambo wa Anti-Balaka ni tishio hasa kwa Waislamu wanaoishi katika kitongoji cha PK 12 huko Bangui, katika miji ya Boda, Carnot na Berberati huko magharibi mwa Bangui na mji wa Bassangoa huko kaskazini.

 Fatoumata Lejeune-Kaba amesema kuwa UNHCR iko tayari kusaidia kuwahamishia Waislamu hao wanaokabiliwa na vitisho vya wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka katika maeneo salama ndani au nje ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.  

0 comments:

Post a Comment