Mwakilishi wa Jimbo la Mji Mkongwe Zanzibar (CUF), Ismail Jussa Landu
amesema ikiwa kweli serikali ya umoja ya kitaifa inataka kuonekana kuwa
inaheshimu utawala bora na haki za binaadamu itende haki kwa kuwapa
dhamana na kuwaachia Masheikh wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya
Kiislamu Zanzibar (JUMIKI) waliowekwa ndani zaidi mwaka sasa.
Masheikh hao waliwekwa ndani tokea mwezi wa 10 mwaka 2012 bila ya
kupewa dhamana kwa madai ya kuhatarisha usalama wa taifa ambapo
Mkurugenzi wa Mshtaka Zanzibar (DPP) alitumia kifungu cha sheria ya
usalama wa taifa katika kujenga hoja ya kuwanyima dhamana watuhumiwa
hayo 10.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa Chama Cha Wananchi (CUF)
uliofanyika huko Chaani, Mkoa wa Kaskazini Unguja, Jussa alisema
Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimesaini mkataba wa kimataifa wa
kuheshimu haki za binaadamu na hivyo inapaswa kuheshimu haki hizo bila
ya kubagua.
Alisema katika katiba zote mbili ya Tanzania na ile ya Zanzibar
katika kifungu cha 18 cha katiba hizo kinampa mtu uhuru wa kutoa maoni
yake na kupokea kwa mujibu wa sheria bila ya kuadhibiwa.
Jussa ambaye ni Mjumbe wa Baraza Kuu Taifa alisema Masheikh wa Uamsho
wamewekwa ndani zaidi ya mwaka sasa bila ya kupewa dhamana wakati
sheria inaipa mahakama uwezo wa kutoa dhamana kwa watuhumiwa wa makosa
yote isipokuwa mauaji na uhaini.
“Ikiwa Zanzibar inataka ionekane kwamba inaheshimu haki za binaadamu
basi iwape dhamana Masheikh hawa maana hata huko kuwaweka ndani bila hata kuwapa dhamana ni kinyume na haki za binaadamu muda umeshakuwa
mwingi wamewekwa ndani bila ya kuzingatia athari za huku katika jamii”
alisisitiza Jussa na kuungwa mkono wa wananchi waliohudhuria katika
mkutano huo.
Katika kitu ambacho kinaonekana kuitia doa Serikali ya Umoja wa
Kitaifa, Jussa alisema ni huko kuendelea kuwaweka ndani Masheikh hao na
kuwanyima dhamana bila wakati sheria inasema huwezi kutiwa hatiani mpaka
kuwepo na ushahidi uliokamilika hivyo kuendelea kuwaweka ni kwenda
kinyume na sheria ambazo Zanzibar wamezipitisha wenyewe.
“Tunasema wapo watu ambao wanaiba na ushahidi upo lakini hawakamatwi
wala hawawekwi ndani na wala hakuna sheria iliyowagusa wapo nje
wanatembea bila ya kuchukuliwa hatua yoyote sasa tunasema mahakimu wa
mwisho ni wazanzibari wenyewe wakiona hakuna haki inayotendeka kwa
Masheikh wao basi wazanzibari wataamua ifikapo 2015” alisema na
kushangiriwa na wananchi wengi kwa kupigiwa makofi.
Kauli hiyo ya Jussa imeungwa mkono na aliyekuwa Mkereketwa wa Chama
Cha Mapinduzi Mohammed Ahmed Sultan (Eddy Riamy) ambaye ametoa wito kwa
serikali ya Umoja wa Kitaifa kuwapa dhamana Masheikh kwani imekuwa kero
kubwa kwa wananchi kila unapopita mitaani.
Mkereketwa huyo ambaye alifuatana na Kamati ya watu sita ya Maridhiano
iliyoongozwa na Mzee Hassan Nassor Moyo, alisema kwamba mbali ya
kukosekana darsa na kusalisha kwa Masheikh hao lakini pia familia zao
zimeathirika kiuchumi na kisaikolojia kutokana na kuwa waume ndio
waliokuwa wakitizama familia na sasa kuwekwa ndani kumeathiri familia
hizo.
Kauli za kutetewa Masheikh hao zimeonekana kuvuta hisia za wananchi
wengi ambapo baadhi yao wlaikuwa wakisema ni wakati mwafaka sasa
Serikali kushughulikia kama ni kuwatia hatiani au kuwapa dhamana lakini
kuendelea kuwaweka rumande kunawanyima haki zao kikatiba na hakuwatendei
haki wao na familia zao.
Jan 5, 2014
Masheikh wapewe dhamana
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment