Sep 27, 2013

Tutarudisha Nauli-FAST JET



KAMPUNI ya ndege ya FastJet imeahirisha uzinduzi wa safari yake kutoka Dar es Salaam kuelekea Johannesburg, Afrika Kusini uliokuwa ufanyike leo, huku ikiahidi kuwarudishia nauli wateja waliokata tiketi kwa ajili ya safari hiyo.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Fastjet, Ed Winter, alisema jana kuwa hali hiyo inatokana na Mamlaka ya Anga ya Afrika Kusini kuomba kupatiwa baadhi ya nakala muhimu kutoka Fastjet kabla ya kuanza kutoa huduma hiyo.

Alisema awali kampuni hiyo ilishakamilisha kila kitu muhimu kilichotakiwa kufanyika, lakini inashangaza kuona dakika ya mwisho wanauliziwa nakala nyingine.

Alieleza kwa mujibu wa Mamlaka za Afrika Kusini itachukua siku kadhaa kuzifanyia kazi taarifa hizo na kutoa kibali hicho kwa kampuni hiyo.

“Hii inakatisha tamaa kwa kuwa hakuna kitu ambacho tulikuwa bado hatujakamilisha, karibu kila kitu kilikuwa tayari na sisi tulijiandaa kuzindua ndege yetu hii.

“Kila kitu kikikamilika Fast Jet itaanza kufanya kazi kila Jumatatu, Jumatano na Ijumaa na kuwa tayari kuongeza huduma zake kadiri mahitaji ya wateja,” alisema Winter.


0 comments:

Post a Comment