Sep 19, 2013

Sakata la Marekebisho ya Muswada wa KATIBA;Wana Siasa Waongo-RAIS KIKWETE



RAIS Jakaya Kikwete ameshangazwa na uongo wa baadhi ya wanasiasa na hasa madai kuwa Rais aliteua wajumbe wa Tume ya Katiba bila kuongozwa na mapendekezo ya wadau mbalimbali waliopendekeza majina hayo.

Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa bado anaendelea kuamini kuwa mchakato wa Katiba Mpya utafikia mwisho mwa mwaka 2014, na hivyo kuiwezesha Tanzania kufanya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 chini ya Katiba Mpya.

Vilevile, Rais Kikwete alisema kuwa hana tatizo na watu wanaopinga sera za Serikali ama hata kumpinga yeye binafsi bali tatizo lake ni wanasiasa na wanaharakati wanaochochea ghasia, fujo na uvunjifu wa amani.

Rais Kikwete aliyasema hayo juzi, mjini San Rafael, California wakati alipokutana na kuzungumza na jumuia ya Watanzania waishio Jimbo la California, Marekani, wakati alipoanza ziara yake ya siku mbili katika jimbo hilo ikiwa ni sehemu ya ziara ya Marekani.

Katika hotuba yake alizungumzia mambo mbalimbali, aligusia mjadala wa karibuni Bungeni kuhusu mchakato wa Katiba Mpya na kusema kuwa alishangazwa na madai kuwa yeye kama Rais hakuongozwa na mapendekezo ya wadau wakati anateua Tume ya Katiba.

“Watu wote niliowateua walipendekezwa na wadau mbalimbali zikiwamo taasisi za dini. Yule Mama Maria Kashonda alipendekezwa na Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Mama Mwantumu Malale alipendekeza Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata). Kila kundi ambalo lilipendekeza watu limepata mjumbe katika tume hiyo wakiwemo walemavu ambao naambiwa nimewasahau.

“Hivi nyie wanasiasa wenzangu mkikosa hoja mnaongopa hata kwa vitu ambavyo viko wazi kabisa. Tulikubaliana kuwa Rais angefanya uteuzi wa wajumbe wa tume baada ya kupokea mapendekezo ya wadau na katika mchakato ulioendeshwa kwa uwazi kabisa. Hivyo, ndiyo ilivyofanyika. 

Sasa uongo wa nini? Kama hakuna hoja ni kwamba hakuna tu na wala uongo hautasaidia,” alisema Kikwete.
Kuhusu kama Tanzania itaweza kupata Katiba Mpya kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Rais Kikwete amesema: “Ningependa sana, na kwa kweli ni matarajio yangu makubwa, kuwa tuweze kumaliza mchakato wetu mwaka 2014 na tuweza kuwa na Katiba Mpya ili iongoze Uchaguzi Mkuu wetu wa mwaka 2015. Mchakato wetu unakwenda vizuri na wala si lazima tuhangaike na Katiba kwa miaka mingi. Muhimu ni ushirikishwaji wa kila mmojawetu.”

0 comments:

Post a Comment