Sep 14, 2013

Mufti ni Msanii-Sheikh Kilemile.



MWENYEKITI wa Kamati Ndogo ya Mazungumzo kati ya Waislamu na Serikali, Sheikh Suleiman Kilemile amedai kuwa Mufti Issa Shaban bin Simba ni msanii katika kupata Mahakama ya Kadhi.
Sheikh Kilemile alisema hatua ya kumuona Mufti Simba msanii imekuja baada ya kujitokeza akiilaumu Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa kupuuza maoni ya Waislamu ya kutaka kuanzishwa kwa mahakama hiyo.

Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari na kuongeza kuwa lawama zilizotolewa na Muft Simba ambaye ni mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), zinashangaza.

“Magazeti kadhaa ya hapa nchini Agosti 31, 2013, yamemkariri Mufti Simba  akilalamika kuwa Waislamu wanapuuzwa kuhusu madai yao ya kutaka Mahakama ya Kadhi hapa nchini.

“Muft Simba ameilaumu Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa kupuuza maoni ya Waislamu ya kutaka kuanzishwa Mahakama ya Kadhi inayotambulika kikatiba hapa nchini,” alisema Sheikh Kilemile.

Alisema lawama zilizotolewa na Muft Simba zinashangaza kwa sababu zaidi ya miaka mitatu iliyopita, Rais Jakaya Kikwete alimuagiza Waziri Mkuu, Mizengo Pinda awasiliane na Bakwata ili kumtaka Simba aunde jopo la masheikh kutoka taasisi mbalimbali za Kiislamu ili liwe chombo cha kuwakilisha Waislamu wote nchini.

“Basi jopo likaundwa kama alivyoagiza waziri mkuu, na hadidu za rejea zikatengenezwa. Kiongozi wa jopo hilo alikuwa Muft Simba.

“Jopo hilo lilikubaliana kwa sauti moja kuwa masuala yote yanayohusu ufuatiliaji wa Mahakama ya Kadhi hapa nchini yatasimamiwa na jopo hilo tu na si vyenginevyo,” alisema.

Alifafanua kuwa baada ya kufanyika kwa vikao vingi chini ya uenyekiti wa Muft na vingine na Pinda mchakato huo ulionesha kufikia hatua nzuri.
Alisema kikao cha mwisho cha jopo hilo chini ya waziri mkuu kilihudhuriwa na baadhi ya watendaji wa Serikali na mawaziri kadhaa wakiwemo Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira,  Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge) William Lukuvi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema.   
“Kwa vile mahakama za kadhi zinapatikana pia katika nchi nyingine za kisekyula kama Uingereza, India, Kenya na hata Zanzibar, Wassira alimshauri waziri mkuu upatikane ujumbe utakaokwenda kutembelea nchi hizo na utakaokusanya wajumbe kutoka serikalini na jopo la masheikh kujionea taratibu za uendeshaji wa mahakama za kadhi katika nchi hizo ili utakaporudi nchini uweze kuelekeza jinsi ya kuziendesha mahakama hizo hapa nchini.
“Pinda alikubali na kuibariki rai hiyo. Aliamuru upande wa jopo la masheikh utoe wajumbe watatu na upande wa Serikali wajumbe wawili. Ilikubaliwa  kuwa gharama za kupeleka ujumbe huo Uingereza, India, Kenya na Zanzibar zilipwe na Ofisi ya Waziri Mkuu.

“Ujumbe huo ulitakiwa uwe umekamilisha ziara hizo kabla ya Aprili mwaka huu wa 2013,” alisema.

Sheikh Kilemile alidai kabla ya kufanikisha hayo, Muft Simba alipuuza yale maazimio ya kikao hicho na badala yake aliamua kuitisha mkutano wa viongozi wa Bakwata mjini Dodoma na kutangaza jina la kadhi wake mkuu pamoja na wasaidizi wake bila kushauriana na jopo la masheikh lililoteuliwa kushughulikia mchakato mzima wa kupatikana Mahakama ya Kadhi.   

“Mtaona alilolifanya Muft Simba ni usanii. Ni kwa sababu hao makadhi aliowateua hawapo kisheria na wala hawana mamlaka yoyote ya kiutendaji,  kisha Sheikh Simba anathubutu kuinyoshea kidole Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Serikali, eti kwa kuwapuuza Waislamu kuhusu Mahakama ya Kadhi,” alisema.


0 comments:

Post a Comment