Apr 23, 2014

Polisi yawapiga ‘stop’ tena Ukawa Zanzibar

Jeshi la Polisi Zanzibar limeendelea kuuchelewesha mkutano wa wanachama wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kwa madai kwamba hakuna askari wa kutosha kuulinda.

Awali, mkutano huo ulipangwa kufanyika Jumamosi iliyopita kwenye Uwanja wa Kibandamaiti, Unguja lakini jeshi hilo liliuzuia kwa madai ya kuwapo kwa habari za kiintelijensia dhidi ya tishio la maisha ya watu.
Awali, Mwenyekiti wa Ukawa, Freeman Mbowe alisema mkutano huo utafanyika leo katika uwanja huo.
Ukawa ni muungano wa vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi, DP na wajumbe 25 kutoka kundi la wajumbe 201 walioteuliwa na Rais Jakaya Kikwete.
Hata hivyo, Msemaji wa Polisi Zanzibar, Mohamed Mhina alisema baadaye kuwa mkutano huo hautafanyika hadi Aprili 30, mwaka huu.
Alisema umezuiwa kwa sababu askari na maofisa wa polisi wanaotakiwa kuusimamia wako Dar es Salaam katika maandalizi ya sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
“Tumekutana nao (CUF walioomba kibali kwa niaba ya Ukawa) na kukubaliana kwamba mkutano huo ufanyike Aprili 30 kwani askari waliopo hivi sasa ni wachache hawawezi kutosha kusimamia ulinzi kutokana na aina ya mkutano wenyewe. 

Hata hiyo siku hiyo hakutakuwapo na maandamano, bali wataruhusiwa kufanya mkutano pekee na siyo vinginevyo.”
Katibu wa Ukawa nje, Shaweji Mketo alisema wamekubaliana na jeshi hilo... “Aprili 30 tutafanya mkutano pale Kibandamaiti na siku inayofuata tutafanya mkutano Pemba.”

0 comments:

Post a Comment