Nov 7, 2013

AU yakosoa UN kwa kupuuza Afrika

Kikao cha Muungano wa Afrika kilichofanyika Addis Ababa mapema mwaka huu

Muungano wa Afrika AU umekosoa baraza la Usalama la Umoja wa mataifa kwa kupuuza sauti za Waafrika katika maamuzi yake.
Mkurugenzi wa Baraza la Amani na Usalama la AU El Ghasim Wane anasema wakati mwingi, baraza la usalama hutoa maamuzi bila kuzingatia maoni ya Muungano huo.

Wane ameonya kuwa huenda mapendekezo ya baraza hili yakapuuzwa, iwapo hali itaendelea kama ilivyo.

Wane alikuwa akizungumza kwenye mkutano uliandaliwa kuangazia suala la ufadhili wa mipango ya usalama na amani barani Afrika, lakini suala tata la uhusiano wa AU na baraza la Usalama la umoja wa mataifa, lilijitokeza.

Mkurugenzi wa baraza la amani na usalama la AU El Ghasim Wane, alisema wakati umefika kwa baraza la usalama la umoja wa Mataifa kusikiza kwa makini sauti ya Afrika.

Tetesi hizo zinajiri huku baadhi ya wanachama wa baraza la Usalama la Umoja wa mataifa wakiripotiwa kupuuza ombi la Umoja wa Afrika la kutaka kesi inayomkabili rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, kusimamishwa kwa muda.

Hata hivyo balozi wa Uingereza katika AU Greg Dorey alisema suala muhimu kuhakikisha kuwa uhusiano wa Umoja wa mataifa na AU unaimarishwa.

Huku akitaka muungano huo kuwa katika mstari wa mbele kutatua baadhi ya changamoto zinazokabili bara hili.

Walikuwa wakizungumza katika mkutano wa kujadili jinsi wafadhili wa kimataifa wanavyoweza kuboresha juhudi za AU kukabiliana na changamoto za kiusalama.

Katika mkutano huo, AU ilikiri kuwa inaweza kufanya vyema zaidi katika kukabiliana na vita kama vile nchini Mali na katika Jamhuri ya Afrika ya kati.

0 comments:

Post a Comment